Mousavi: Wadau wote duniani wana mchango katika zama za baada ya Magharibi
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza kuwa: "Hivi sasa, sisi tunaishi katika dunia ya baada ya enzi za Magharibi, ambapo wadau wote duniani wana mchango katika mahusiano ya zama hizo."
Sayyed Abbas Mousavi ameyasema hayo akiashiria mazoezi ya pamoja ya kijeshi ya vikosi vya Wanamaji vya Iran, Russia na China yanayoendelea kufanyika kaskazini ya Bahari Kuu ya Hindi na Bahari ya Oman.
Katika ujumbe aliotuma kwenye ukurasa wake wa kijamii wa Twitter, Mousavi ameandika kuwa, katika dunia ya leo ile hali ya kwamba, kila jambo kubwa lazima lifanywe na Magharibi au litokee huko haipo tena.
Manuva ya pamoja ya majeshi ya Wanamaji ya Iran, Russia na China yakiwa na ujumbe wa "Amani, Urafiki na Usalama Endelevu Chini ya Kivuli cha Ushirikiano na Muungano wa Pamoja", yalianza jana katika eneo la kaskazini ya Bahari Kuu ya Hindi na Bahari ya Oman na yataendelea hadi siku ya Jumatatu.
Katika luteka hiyo, vikosi vya wanamaji wa nchi hizo tatu vinafanya mazoezi ya mbinu mbali mbali za kijeshi ikiwemo uokoaji wa meli iliyoshika moto, kukomboa meli iliyovamiwa na kutungua shabaha walengwa maalumu baharini.
Mazoezi hayo ya kijeshi yameakisiwa sana na vyombo mbali mbali vya habari duniani.../