Feb 16, 2021 03:35 UTC
  • Rouhani: Usalama na amani ya Asia Magharibi vitaimarishwa kupitia ushirikiano wa nchi za eneo

Rais Hassan Rouhani wa Iran amesema amani na usalama katika eneo la Asia Magharibi vinaweza kuimarishwa tu kupitia ushirikiano wa mataifa ya eneo hili na wala si kwa uingiliaji wa madola ajinabi.

Rais Rouhani alisema hayo jana Jumatatu hapa mjini Tehran katika mazungumzo yake na Sheikh Mohammed bin Abdulrahman Aal-Thani, Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar ambapo amesisitiza pia haja ya kuimarishwa uhusiano wa pande mbili wa Doha na Tehran katika nyuga mbalimbali.

Dakta Rouhani  amesema Iran na Qatar zinaweza kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa pande mbili katika nyuga mbalimbali kama vile uchumi, biashara, utalii, utamaduni na sayansi; sambamba na ushirikiano wa karibu wa sekta za kibinafsi za mataifa haya mawili.

Rais wa Iran amegusia kuhusu ujio wa utawala mpya nchini Marekani na hamu ya serikali ya Joe Biden ya kuirejesha Washington katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA na kueleza bayana kuwa: Mara tu Marekani itakapoiondolea Iran vikwazo haramu na kurejea katika Azimio Nambari 2231 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Jamhuri ya Kiislamu itarejea mara moja katika utekelezaji wa wajibu wake katika mapatano hayo.

Amesema hii leo imethibiti kwa dunia kuwa sera ya mashinikizo ya kiwango cha juu kabisa imefeli na serikali mpya ya Marekani haina chaguo jingine ghairi ya kusahihisha makosa ya utawala uliopita wa Donald Trump, na kutekeleza wajibu wake wa kisheria.

Jumbe za Iran na Qatar zikiongozwa na Waziri Zarif na Bin Jassim Aal-Thani mjini Tehran

Kwa upande wake, Sheikh Mohammed bin Abdulrahman Aal-Thani, Waziri wa Mambo ya Nje wa Qatar ameitaja Iran kama nchi rafiki katika eneo, na kutoa mwito wa kuimarishwa uhusiano na ushirikiano wa pande mbili katika nyuga tofauti hususan uga wa biashara na uchumi.

Huku akiashiria kuwa Iran ni taifa lenye nguvu na ushawishi mkubwa katika eneo, Mohammed bin Abdulrahman bin Jassim Aal Thani amebainisha kuwa, "daima tunadiriki umuhimu wa kuimarisha usalama, amani na uthabiti miongoni mwa nchi za eneo, na kupatia ufumbuzi migogoro na tofauti zilizopo kupitia njia za mazungumzo na mikakati kama mpango wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wa Ubunifu wa Amani ya Hormuz, HOPE."

Hapo jana pia, Mohammad Javad Zarif, Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran alikutana na kufanya mazungumzo na mwenzake huyo wa Qatar kuhusu uhusiano wa pande mbili, masuala ya kieneo na kimataifa.

Tags