Amir Abdollahian: Azimio la UN haliizuia Iran kuuza silaha nje ya nchi
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i90440-amir_abdollahian_azimio_la_un_haliizuia_iran_kuuza_silaha_nje_ya_nchi
Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran amesema: "Kwa mujibu wa azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama, hakuna marufuku ya kuagiza na kuuza silaha za Iran nje ya nchi, na Tehran haijaipa Russia silaha zozote ili zitumike katika vita vya Ukraine."
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Nov 12, 2022 08:10 UTC
  • Amir Abdollahian: Azimio la UN haliizuia Iran kuuza silaha nje ya nchi

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran amesema: "Kwa mujibu wa azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama, hakuna marufuku ya kuagiza na kuuza silaha za Iran nje ya nchi, na Tehran haijaipa Russia silaha zozote ili zitumike katika vita vya Ukraine."

Ikumbukwe kuwa, katika wiki za hivi karibuni, maafisa wa Marekani na nchi za Ulaya wamekuwa wakidai kuwa Iran ilituma ndege zisizo na rubani nchini Russia ili zitumiwe katika vita dhidi ya Ukraine.

Maafisa wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran wamekanusha madai hayo, lakini Wamagharibi bado wanasisitiza juu ya madai yao yasiyo na msingi.

Kuhusiana na hilo, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran Hossein Amir Abdollahian amesisitiza katika mazungumzo ya simu na mwenzake wa Bulgaria, Nikolay Milkov, kwamba: Azimio nambari 2231 la Baraza la Usalama haliipiga marufuku Iran kusafirisha na kuagizaji silaha lakini pamoja na hayo Tehran haijaipatia Russia silaha zozote za kutumiwa katika vita vya Ukraine.

Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Iran amesema: "Msimamo wetu ni dhidi ya upanuzi wa NATO katika eneo la Mashariki na dhidi ya vita vya Ukraine, na tunafanya kazi kwa ajili ya kusitisha mapigano."

Amir Abdollahian pia ametoa shukurani zake kwa msimamo wa Bulgaria wa kulaani shambulizi la kigaidi la ISIS katika haram ya Hazrat Shah Cheragh (as) huko Shiraz na kusisitiza umuhimu wa uhusiano wa pande mbili wakati huu wa kuadhimisha miaka 125 ya uhusiano wa kidiplomasia kati ya nchi hizo mbili.

Kwa upande wake, Nikolay Milkov amemshukuru Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa maelezo yake kuhusiana na matukio ya Ukraine na msimamo wa Iran wa kupinga vita na kutafuta suluhisho la kisiasa la mgogoro wa Ukraine na kuongeza kuwa: Serikali ya Bulgaria inaunga mkono mchakato wa kuhuisha mapatano ya nyuklia ya JCPOA na kufikiwa mapatano kati ya Iran na jamii ya kimataifa.