Jan 19, 2023 10:26 UTC
  • Israel yashadidisha ukatili wake dhidi ya Wapalestina Ukingo wa Magharibi

Wanajeshi makatili wa utawala wa Kizayuni wa Israel wameshambulia kambi ya wakimbizi ya Wapalestina katika mji wa Jenin, kaskazini mwa eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan linalokaliwa kwa mabavu, na kuua shahidi Wapalestina wawili.

Vyombo vya habari vya Palestina vimeripoti habari hiyo na kueleza kuwa, vikosi vya utawala haramu wa Israel mapema leo vimevamia kambi hiyo ya wakimbizi na kupelekea kuzuka makabiliano baina yao Wapalestina wakazi wa eneo hilo.

Habari zaidi zinasema kuwa, Wapalestina wawili waliouawa shahidi katika muendelezo huo wa chokochoko za Wazayuni ni Jawad Bawatqa aliyekuwa na umri wa miaka 58 na Adham Jabarin aliyekuwa na miaka 26.

Inaarifiwa kuwa, Bawatqa, ambaye alikuwa mwalimu wa shule, ameuawa kwa kupigwa risasi na mlengaji shabaha wa Kizayuni. Jabarin alikuwa mmoja wa makamanda wa Brigedi za Mashahidi wa al-Aqsa.

Duru rasmi zinaarifu kuwa, kuuawa shahidi wawili hao mapema leo Alkhamisi kunafikisha idadi ya Wapalestina waliouawa kinyama na askari wa Kizayuni mwaka huu 2023 kufikia 17, wakiwemo watoto wanne.

Kwa mujibu wa takwimu za Wizara ya Afya ya Palestina, Wapalestina karibu 200 waliuawa shahidi na jeshi katili la Israel huko Ukingo wa Magharibi na katika Ukanda wa Gaza mwaka uliomalizika 2022.

Katika miezi ya hivi karibuni, askari makatili wa utawala wa Kizayuni wameshadidisha ukatili na jinai zao dhidi ya Wapalestina hususan katika miji ya Jenin na Nablus eneo la Ukingo wa Magharibi linalokaliwa kwa mabavu. Hata hivyo wanamuqawama wa Palestina wamejibu mapigo kwa kutekeleza operesheni kadhaa dhidi Wazayuni katika eneo hilo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, na kuangamiza Wazayuni kadhaa.

 

Tags