Mwandishi wa Israel: Wazayuni 1,815 wamengamizwa na Hamas
Yossi Milman mwandishi habari mtajika Mzayuni ameandika katika ukurasa wake wa X, Twitter ya zamani, kwamba hadi sasa Wazayuni 1,815 wameuawa katika mashambulizi ya wanamapambano wa Hamas.
Yossi Milman mwandishi wa habari na ripota wa masuala ya usalama wa Kizayuni aliandika jana katika ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa X kwamba: Hadi sasa Wazayuni 1,815 wameangamizwa katika mashambulizi ya wanamapambano wa Izzudin Qassam, tawi la kijeshi la Hamas; na kwamba utambulisho wa 455 miongoni mwao bado haujajulikana.
Milman ameongeza kuwa, Wazayuni 1,000, wanajeshi 291, maafisa 10 wa Shirika la Usalama la Israel, (Shin Bet) na maafisa polisi 54 ni miongoni mwa Wazayuni walioangamizwa katika Oparesheni ya Kimbunga cha Al Aqsa. Wakati huo huo, maafisa wa polisi 50 wa Kizayuni hawajulikani walipo.
Katika upande mwingine, huku kukiripotiwa habari kuhusu kuongezeka idadi ya majeruhi katika jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel na kuangamizwa wanajeshi 286 wa utawala huo ghasibu kwa mujibu wa takwimu rasmi; Kanali ya 10 ya Wazayuni ilitangaza juzi katika siku ya kumi ya oparesheni ya Kimbunga cha Al Aqsa kwamba: Wanajeshi wengi wa Israel wamekimbia jeshini wakipinga kushiriki katika mashambulizi dhidi ya Ukanda wa Ghaza.
Kanali ya 10 ya utawala wa Kizayuni imeongeza kuwa, kumeibuka hitilafu na mvutano mkubwa kati ya viongozi na maofisa wa jeshi la utawala wa Kizayuni na kuna taarifa kwamba, baadhi ya maofisa wa ngazi ya juu wa jeshi wamekataa kushiriki katika mashambulizi dhidi ya Ghaza.