Israel yaua shahidi Wapalestina 4 Jenin, Ukingo wa Magharibi
Vijana wanne wa Kipalestina wameuawa shahidi kwa kupigwa risasi na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel katika mji wa Jenin, kaskazini ya eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Shirika la habari la Palestina la Wafa limeripoti habari hiyo na kuongeza kuwa, wanajeshi wa Kizayuni wamefanya mauaji hayo leo Jumapili, sambamba na kuzingira hospitali za Shahidi Khalil Suleiman na Ibn Sina katika eneo hilo linalokaliwa kwa mabavu.
Wafa imemnukuu Mkurugenzi wa Hospitali ya Al-Razi akiwatambua wahanga wa jinai hizo za Israel Ukingo wa Magharibi kuwa Ammar Muhammad Abu al-Wafa (21), Ahmed Abu al-Hija (20), Muhammad Mahmoud Fraihat (27) na Mahmoud Khaled Abu al-Hija (17).
Katika hatua nyingine, Idara ya Wafungwa wa Palestina imethibitisha habari ya jeshi la Kizayuni kuwaachia huru wafungwa wengine 39 wa Kipalestina mkabala wa kuachiwa mateka 17 wa Gaza (Waisraeli 13 na raia 4 wa Thailand).
Kabla ya hapo, jeshi la Kizayuni liliwaachia huru wafungwa wengine, ambao ni wanawake 24 na watoto 15, kama sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya kusitisha mapigano.
Usitishaji vita wa siku nne kati ya utawala wa Kizayuni na Harakati ya Muqawama ya Palestina Hamas ulianza kutekelezwa juzi Ijumaa asubuhi, baada ya Wazayuni kuwaua shahidi Wapalestina zaidi ya 15,000.
Utawala huo umekubali kushindwa katika operesheni yake ya kuwakomboa mateka na kusalimu amri mbele ya matakwa ya Wapalestina.
Wanamuqawama wa Palestina walianzisha Operesheni ya Kimbunga cha Al-Aqsa dhidi ya utawala ghasibu wa Israel mnamo Oktoba 7, ikiwa ni katika kukabiliana na zaidi ya miongo saba ya uvamizi wa utawala huo dhidi ya watu wa Gaza na maeneo mengine ya ardhi zinazokaliwa kwa mabavu.