Israel yaendelea kumwaga damu za watoto wadogo Jenin
Watoto wawili wa Kipalestina wameuawa shahidi kwa kupigwa risasi na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel katika mji wa Jenin, kaskazini ya eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Wizara ya Afya ya Palestina imewatambua watoto hao waliouawa shahidi jana Jumatano katika uvamizi wa wanajeshi makatili wa Israel katika eneo hilo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu kuwa ni Adam Samer al-Ghoul (8) na Basil Suleiman Abu al-Wafa (15).
Shirika la habari la Palestina la Wafa limeripoti kuwa, wanajeshi wa Kizayuni mbali na kutekeleza mauaji hayo ya kinyama, lakini pia wameharibu nyumba kadhaa na miundimbinu katika eneo hhilo, na vile vile wameshambulia nyumba moja kwa kuipiga bomu kwa kutumia droni.
Kwa mujibu wa kanali ya televisheni ya al-Mayadeen ya Lebanon, askari wa utawala ghasibu wa Israel wamewatia mbaroni familia nyingi katika mji wa Jenin katika uvamizi wake huo.
Haya yanajiri siku chache baada ya vijana wanne wa Kipalestina kuuawa shahidi kwa kupigwa risasi na jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel katika mji huo wa Jenin, Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Wahanga wa jinai hizo za Israel Ukingo wa Magharibi ni Ammar Muhammad Abu al-Wafa (21), Ahmed Abu al-Hija (20), Muhammad Mahmoud Fraihat (27) na Mahmoud Khaled Abu al-Hija (17).
Gazeti la Kizayuni la Yediot Aharonot limezinukuu duru za kijeshi zikisema kwamba, makadirio ya jeshi la Kizayuni yanaonyesha kuwa, wapiganaji wa muqawama mjini Jenin wanajaribu kurejesha nguvu na uwezo wao wa kijeshi baada ya operesheni za hivi karibuni na wamejikita zaidi kwenye miundombinu na kutengeneza mabomu ya mkono