Yair Golan: 'Serikali Sifuri' ya Netanyahu inaiburuza Israel kwenye vita visivyo na mwisho
Sep 16, 2024 03:37 UTC
Kiongozi wa upinzani katika utawala wa Kizayuni wa Israel Yair Golan ameutaja muungano unaotawala wa waziri mkuu Benjamin Netanyahu kuwa "serikali sifuri" ambayo inaupeleka utawala huo kwenye "vita visivyo na mwisho."
Kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Kizayuni, watu wapatao tisa walijeruhiwa baada ya kombora la balestiki lililorushwa kutokea Yemen kutua karibu na Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Ben Gurion mjini Tel Aviv mapema jana Jumapili.
Katika ujumbe alioandika kwenye mtandao wa kijamii wa X, Golan, ambaye anaongoza chama cha Leba, ametoa wito kwa Waisraeli kufanya maandamano ya kila siku dhidi ya serikali.
Amesema: "ni mashinikizo ya wananchi tu ndiyo yatakayoweza kuiangusha serikali hii".
Kiongozi huyo wa upinzani katika utawala bandia wa Israel ameeleza kwamba shambulio la kombora la Jumapili linakumbusha namna serikali ya mrengo wa kulia inavyoendelea kushindwa.
Golana ameongeza kuwa, badala ya kufunga medani za mapigano, serikali hiyo ya sifuri inawaburuza Waisraeli kwenye vita visivyoisha, migogoro ya milele ya ndani na shimo lenye kina kisicho na mwisho.
Chama cha Yesh Atid kinachoongozwa na kiongozi mwingine wa upinzani Yair Lapid nacho pia kimetoa taarifa ya kutaka serikali ya Netanyahu ijiuzulu, ikiita "serikali ya majanga ya kitaifa".../