Askari wa Israel waziporomosha kwa mateke maiti za Wapalestina kutokea kwenye paa la jengo
(last modified 2024-09-20T07:40:59+00:00 )
Sep 20, 2024 07:40 UTC
  • Askari wa Israel waziporomosha kwa mateke maiti za Wapalestina kutokea kwenye paa la jengo

Askari katili wa jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel wamedhihirisha tena unyama wao baada ya kunaswa kupitia mkanda wa video wakiziporomosha kwa mateke maiti za Wapalestina waliowaua katika shambulio walilofanya katika eneo la Qabatiya, Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan unaokaliwa kwa mabavu.

Katika shambulio hilo la jana Alkhamisi lililochukua muda wa saa kadhaa, askari wa utawala wa Kizayuni waliwaua shahidi Wapalestina watano katika eneo hilo.

Katika upande mwingine, shirika la habari la Palestina Wafa limeripoti kuwa, vikosi vya jeshi la utawala wa Kizayuni vimevamia kijiji cha Palestina cha Amatin, karibu na Qalqilya katika Ukingo wa Magharibi na kuwakamata ndugu watatu.

Mbali na Ghaza, jeshi la Israel linafanya mashambulizi na mauaji Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan pia

Wanajeshi wa Israel wamefanya uvamizi mkali pia huko Qalandiya, karibu na Ramallah, na kumpiga risasi na kumjeruhi vibaya mtu mmoja.

Uvamizi wa jeshi la Kizayuni umefanywa pia katika vitongoji kadhaa vya Nablus lakini hakuna majeruhi au watu waliokamatwa kufikia sasa.

Wakati huohuo, Ulinzi wa raia katika Ukanda wa Ghaza umeripoti kuwa Wapalestina wengine 12 wameuawa shahidi katika mashambulizi mawili yaliyofanywa na jeshi la Israel kwenye mji wa Ghaza baada ya hujuma za kijeshi za utawala huo ghasibu kupelekea kuuawa watu 28 katika eneo hilo hapo jana.../

 

Tags