Russia: Marekani ingali inaiba mafuta na ngano ya Syria
Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Russia amesema kuwa, Marekani inaendelea kuiba na kutorosha mafuta na ngano ya Syria.
Sergei Vershinin jana alikiambia kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kilichodali hali ya Syria kwamba, misafara ya wanajeshi wa Marekani kila siku inaiba na kutorosha mafuta na ngano inayozalishwa nchini Syria na kuipeleka Iraq.
Vershinin ameongeza kuwa, Wamarekani wanaendelea kuiba na kufanya magendo ya mafuta na ngano ya Syria huku watu wa Syria wenyewe wakisumbuliwa na uhaba wa chakula.

Naibu Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje wa Russia amesema kuwa, magendo ya mafuta na ngano ya Syria inafanywa kila siku na wanajeshi wa Marekani na kuongeza kuwa, ripoti zinazonyesha kuwa, tarehe 23 mwezi huu wa Machi pekee karibu magari makubwa 300 ya kubeba mafuta na mengine zaidi ya 200 ya ngano yalitoroshwa na askari wa Marekani kutoka Syria na kupelekwa Iraq.