Umoja wa Mataifa wakosolewa kwa kuupendelea muungano vamizi wa Saudia
Viongozi wa Serikali ya Wokovu wa Kitaifa ya Yemen wamekosoa vikali kile walichokitaja kuwa, hatua za Umoja wa Mataifa za kuupendelea muungano vamizi unaoongozwa na utawala wa Saudi Arabia.
Viongozi wa Yemen wanasisitiza kuwa, hatua ya mjumbe mpya wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen ya kuupendelea muungano vamizi wa Saudia haina natija nyingine ghairi ya kuzidi kuurefusha mgogoro wa Yemen.
Jalal al-Rowaishan, Naibu Waziri Mkuu wa Yemen amesema katika radiamali yake kwa matamshi ya Hans Grundberg, mjumbe mpya maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen amesema, ripoti ya mwakilishi huyo wa UN inauonyesha upande ulioanzisha vita dhidi ya Yemen na kulizingira taifa hilo kuwa eti ndio uliodhulumiwa.
Naibu Waziri Mkuu wa Yemen amesisitiza kuwa, kama Umoja wa Mataifa una nia ya kweli ya kuhitimisha vita nchini Yemen, basi unapaswa kuchukua maamuzi yake bila ya kushawishiwa au kushinikizwa na madola makubwa.
Wakati huo huo, Abdel-Aziz bin Habtour, Waziri Mkuu wa Yemen naye amesema katika radiamali yake kwa matamshi ya Hans Grundberg, mjumbe mpya maalumu wa Umoja wa Mataifa katika masuala ya Yemen kwamba, upande uliofanya uvamizi dhidi ya Yemen ni Saudi Arabia na Imarati na ndege zinazofanya mashambulio na kuuawa wananchi wa Yemen zinanyanyuka na kupaa kutoka katika ardhi za mataifa hayo.
Hii sio mara ya kwanza kwa viongozi wa Serikali ya Wokovu wa Kitaifa ya Yemen kukosoa utendaji usiofaa wa Umoja wa Mataifa kuhusiana na mgogoro wa Yemen, ambapo licha ya malalamiko hayo, maafisa wa umoja huo wameendelea kuwa watumwa wa madola ya kibeberu.