Trump: Hillary Clinton ni mzizi wa matatizo ya kiusalama duniani
Mgombea wa kiti cha rais kwa tiketi ya chama cha Republican nchini Marekani, Donald Trump amesema aghalabu ya changamoto za kiusalama zinaoikabili dunia kwa sasa zilisababishwa na hasimu wake wa kisiasa Hillary Clinton, anayetaka kuwa rais kupitia chama cha Democrats.
Trump aliyasema hayo jana katika mji wa Cleveland jimbo la Ohio alipokuwa akitoa hotuba ya kukubali rasmi uteuzi wa yeye kubeba bendera ya Republican katika uchaguzi wa rais nchini humo na kuongeza kama tunavyomnukuu: "Jina la Clinton likitajwa, mambo ambayo yanakuja akilini ni vifo, uharibifu, ugaidi na udhaifu. Waziri wa Mambo ya Nje wa zamani ni mtumwa wa mabwanyeye fulani waliomdhibiti huko nyuma na wanaofadhili kampeni zake za sasa na kwa msingi huo hawezi kuwaletea Wamarekani mabadiliko yoyote."
Hii ni katika hali ambayo, katika miezi ya hivi karibuni Donald Trump kwa upande wake amekuwa akitoa matamshi ya kibaguzi na kichochezi dhidi ya Uislamu na Waislamu pamoja na wahamiaji nchini humo. Disemba mwaka jana alitoa wito wa kuzuiwa Waislamu kuingia katika ardhi ya Marekani.
Haya yanajiri wiki moja baada ya matokeo ya uchunguzi wa maoni uliofanywa na shirika la Associated Press na JFK kuonyesha kwamba asilimia 81 ya Wamarekani wana wasiwasi mkubwa wa kuchaguliwa kwa Hillary Clinton na Donald Trump kuwa marais wa nchi hiyo.
Uchaguzi wa rais nchini Marekani umepangwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.