Jumuiya ya Mabunge yalaani jinai dhidi ya Waislamu wa Mynamar
Jumuiya ya Mabunge imelaani mauaji na jinai dhidi ya Waislamu Warohingya wa Myanmar katika kikao chake huko Saint Petersburg nchini Russia mkutano ambao umefanyika kwa ubunifu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Katika siku ya pili ya mkutano huo, washiriki wamepasisha azimio la kulaani mauaji ya kizazi yanayofanywa na jeshi la Myanmar likishirikiana na Mabudha wenye misimamo ya kufurutu ada dhidi ya Waislamu Warohingya wa Myanmar.
Azimio hilo lililopasishwa kwa wingi wa kura lilipendekezwa na nchi za Iran, Bangladesh, Imarati, Morocco, Uturuki, Sudan na Indonesia. Kwa mujibu wa azimio hilo, suala la jamii ya kimataifa kuhitimisha mgogoro wa kibinadamu wa Myanmar limetiliwa mkazo.
Aidha kusitishwa kamata kamata na mashambulio ya kinyama dhidi ya Waislamu Warohingya na kutajwa mashambulio hayo kuwa yanatishia usalama na amani ya kimataifa na vile vile kuhakikishiwa usalama raia wa Kirohingya waliokimbia makazi yao mara watakaporejea makwao ni vipengee vingine vya azimio hilo.
Maelfu ya Waislamu wa kabila la Rohingya nchini Myanmar wameuawa na maelfu ya wengine kujeruhiwa tangu kuanza wimbi jipya la mashambulizi ya jeshi na Mabudha wenye misimamo mikali katika mkoa wa Rakhine magharibi mwa nchi nchi hiyo tangu tarehe 25 Agosti mwaka huu hadi sasa. Mauaji hayo ya umati dhidi ya Waislamu nchini Myanmar yamepelekea zaidi ya nusu milioni kati yao kukimbilia hifadhi katika nchi jirani ya Bangladesh.