Mgongamno katika madai ya Marekani ya kutoka nchini Syria
Marekani imeendelea kutoa matamshi yanayogongana baada ya Ikulu ya nchi hiyo (White House) kudai kuwa rais wa nchi hiyo Donald Trump amekusudia kuwaondoa haraka wanajeshi wa nchi hiyo walioko Syria.
Shirika la habari la Reuters limemnukuu msemaji wa White House, Sarah Sanders, akisema kuwa, misimamo ya nchi yake haijabadilika na kwamba rais wa nchi hiyo, Donald Trump amesema wazi kuwa amekusudia kuwaondoa wanajeshi wa Marekani nchini Syria haraka iwezekanavyo.
Wakati huo huo Nikki Halley, mwakilishi wa Marekani katika Umoja wa Mataifa jana usiku alisema kuwa wanajeshi wa Marekani watabakia nchini Syria na hawataondoka nchini humo hadi malengo ya Washington yatakapotimia.
Naye rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron amesema kuwa ameikinaisha Marekani ibakie kwa muda mrefu nchini Syria.
Matamshi ya kugongana ya viongozi wa Marekani kuhusu kuondoka nchini Syria yametolewa katika hali ambayo Uingereza na Ufaransa, alifajiri ya siku ya Jumamosi zilishirikiana na Marekani kufanya mashambulizi katika baadhi ya maeneo ya Syria kwa madai yasiyothibitishwa ya kuwa serikali ya nchi hiyo imetumia silaha za kemikali katika mji wa Douma wa Ghaouta Mashariki.