Ufaransa yamkosoa Trump, yasema ni mtu mwenye migongano
Ofisi ya Rais wa Ufaransa imetangaza kuwa mienendo ya Rais Donald Trump wa Marekani katika mkutano wa nchi saba zilizopiga hatua kiviwanda maarufu kama G7 si thabiti na inagonga na kukinzana.
Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Rais wa Ufaransa imesema kuwa, katika kikao chao cha siku mbili nchini Canada, viongozi wa G7 walitayarisha na kutia saini hati ya mwisho ambayo inapaswa kuheshimiwa, na kila mtu asiyeitekeleza na kuiheshimu ana shakhsia kigeugeu na yenye migongano.
Jana Jumapili Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa alijibu msimamo wa Rais Donald Trump wa Marekani wa kuondoa saini yake katika taarifa ya mwisho ya G7 kwa kusema kuwa, "hasira na ghadhabu haviwezi kuzitwisha nchi nyingine mitazamo na matakwa yake katika masuala ya ushirikiano wa kimataifa".
Baada ya kuondoka katika kikao cha viongozi wa G7, Rais Donald Trump wa Marekani alimkosoa vikali mwenyeji wa mkutano huo, yaani Waziri Mkuu wa Canada, Justin Trudeau akimtaja kuwa ni mtu dhaifu na akaondoa saini yake katika taarifa ya mwisho ya mkutano huo.
Hatua hiyo ya Trump imokosolewa sana na viongozi wa nchi nyingine walioshiriki mkutano huo.