Mawaziri wa G20 wataka mabadiliko WTO kukabiliana na uhasama wa Marekani
Mawaziri wa biashara na uwekezaji wa nchi tajiri duniani za kundi la G20 wamesema kuna haja ya kufanyika mabadiliko ya dharura katika Shirika la Biashara Duniani WTO kukabiliana na vita vya kibiasahra vya Marekani dhidi ya China.
Katika taarifa ya pamoja, mawaziri hao wamesema wameimarisha mikakati ya kufanya mazungumzo kuhusu migogoro ya kimataifa ya biashara ingawa hawakutaja moja kwa moja ni vipi mabadiliko yatafanyika katika WTO.
Marekani imetangaza vita vya kibiashara dhidi ya Marekani kwa kuweka ushuru mpya wa forodha wenye kugharimu dola bilioni 200 kwa bidhaa zinazotengenezwa nchini China. Marekani pia imeongeza ushuru wa forodah kwa bidhaa zinazotoka Umoja wa Ulaya na Canada.

Katika mkutano huo wa mawaziri wa nchi za G20 ambao umefanyika nchini Argentina, waandamanaji siku ya Jumamosi waliteketeza moto bendera za Marekani huku wakitoa nara dhidi ya Rais Donald Trump wa nchi hiyo. Tayari Trump ametishia kuwa atajiondoa WTO huku China ikitaka marekebisho katika shirika hilo la biashara duniani ili kuleta usawa katika biashara ya kimataifa.