Waziri Mkuu wa Ufaransa akiri kupuuzwa matakwa ya wananchi
Kufuatia maandamano ya wananchi wa Ufaransa wanaolalamikia matatizo ya kiuchumi na kuupinga mfumo wa kibepari nchini humo, Waziri Mkuu wa nchi hiyo amesema kuwa serikali imefanya makosa na haijatoa uzito wa kutosha kwa matakwa ya wananchi.
Edouard Philippe amesema katika mahojiano na gazeti la Les Echos (Lazako) kwamba, kumejadiliwa suala la kufanyika kura ya maoni ambayo inaweza kuwa wenzo mzuri kwa demokrasia. Kufanyika kura ya maoni kwa lengo la kutekeleza marekebisho katika serikali ya Ufaransa ni miongoni mwa matakwa ya raia wanaoandamana na wanaharakati wanaopinga ubepari nchini Ufaransa.
Rais Emmanuel Macron wa Ufaransa ametoa ahadi kadhaa katika jitihada za kupunguza malalamiko ya wananchi na wachumi wanakadiria kuwa, kunahitajika kiasi cha yuro bilioni 15 ili kuweza kutekeleza mipango hiyo.
Wakati huo huo Waziri Mkuu wa Ufaransa, Edouard Philippe amesema nakisi ya bajeti ya nchi hiyo imeongezeka kwa asilimia 3.20 katika uzalishaji wa ndani.
Karibu watu elfu 66 wamlimiminika mitaani nchini Ufaransa tarehe 15 mwezi huu katika awamu ya tano ya maandamano ya wanaharakati waliopata umaarufu kama wavaaji wa vizibao vya njao. Maandamano hayo yalianza kupinga ongezeko la ushuru wa mafuta ya dizeli nchini humo.