Trump alitaka kumtimua mwanawe na mkwewe White House
Kitabu kilichochapishwa hivi karibuni kabisa kimefichua kwamba mwaka 2017 rais wa Marekani Donald Trump alitaka kuwatimua katika Ikulu ya nchi hiyo White House, mwanawe Ivanka Trump na mumewe Jared Kushner kutokana na makelele waliyoyaanzisha tangu Trump aingie White House.
Gazeti la kila wiki la People lilifichua jana Jumatano kwamba Ivanka Trump, binti wa Donald Trump na mumewe Jared Kushner ambao wote wawili ni washauri wakuu wa Trump, wamesababisha makelele na kashfa nyingi tangu waingie katika Ikulu ya Marekani, White House.
Katika kitabu kipya kilichoandikwa na Vicky Ward kwa jina la "Kushner, Inc.: Greed. Ambition. Corruption." mwandishi huyo amefichua kwamba mambo mengi yaliyojificha kuhusu maisha ya Jared Kushner na mkewe Ivanka Trump.
Sehemu moja ya kitatu hicho inasema kuwa, Donald Trump alimtaka John Kelly, mkuu wa zamani wa wafanyakazi wa White House awatimue mwanawe na mumewe kwenye ikulu hiyo.
Kwa mujibu wa mahojiano aliyofanyiwa mwandishi wa kitabu hicho Vicky Ward, karibu watu 220 ambao wengi wao hawakupenda kutajwa majina yao wamethibitisha habari hiyo na kusema kwamba mwaka 2017 Trump alikuwa anamwambia John Kelly kuwa: "Wafukuze wanangu hapa na uwarejeshe New York kwa sababu hawajui jinsi ya kucheza mchezo ninaoucheza."
Hayo yamejiri katika hali ambayo, msemaji wa White House, Sara Sanders, amejibu haraka yaliyoandikwa kwenye kitabu hicho akisema kuwa, inasikitisha kuona kuwa vyombo vya habari vinaacha kazi zao na kukivalia njuga kitabu ambacho maneno yake yanategemea watu wasiojulikana.