Katibu Mkuu wa UN: Tuna deni kubwa kwa wananchi wa Afghanistan
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema kuhusu mustakabali wa kibinadamu nchini Afghanistan ya kwamba suala muhimu si kile ambacho watapatiwa wananchi wa taifa hilo bali deni la jamii ya kimataifa kwa wananchi wao.
Guterres ameyasema hayo, alipohutubia mkutano juu ya mustakabali wa hali ya kibinadamu ya Afghanistan uliofanyika kwa njia ya mtandao na ukumbini jijini Geneva Uswisi na New York Marekani na kuhudhuriwa pia na wakuu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa kama lile la kuhudumia watoto UNICEF na la misaada ya kibinadamu, OCHA.
Katibu Mkuu wa UN amesema “baada ya miongo ya vita, machungu na ukosefu wa usalama, hivi sasa wananchi wa Afghanistan wanakabiliwa na saa hatari zaidi na huu ni wakati wa jamii ya kimataifa kuonesha mshikamano nao.”
Akichambua hali ya sasa Afghanistan, Guterres amesema mwananchi 1 kati ya 3 hawana uhakika wa mlo ujao, umaskini umeshamiri na huduma za msingi za umma zinakaribia kuporomoka kabisa huku ugonjwa wa Corona au COVID-19 ukiendelea kukabili nchi hiyo.
Amesema ingawa Umoja wa Mataifa na wadau wa kibinadamu wanaendelea kutoa misaada kwa wananchi ikiwemo chakula na huduma za afya huku mamlaka za Watalibani zikiahidi ushirikiano kuhakikisha misaada inafikishwa kwa wananchi bado kuna mambo makuu manne ya kuzingatia.
Ametaja mambo hayo kuwa ni pamoja na fedha, kuimarishwa kwa uwezo wa kufikisha misaada ya kibinadamu ikiwemo kwa njia ya anga kati ya mji mkuu Kabul na maeneo mengine nchini humo, kulinda haki za wanawake na wasichana Afghanistan ikiwemo kupata elimu na huduma nyingine za msingi na vilevile kuhakikisha kuwa huduma za usaidizi wa kibinadamu siyo tu zinaokoa maisha bali pia zinaokoa mbinu za kujipatia kipato.../