IMF na Benki ya Dunia zafanya mikutano ya kwanza barani Afrika katika kipindi cha miaka 50
(last modified 2023-10-10T15:02:10+00:00 )
Oct 10, 2023 15:02 UTC
  • IMF na Benki ya Dunia zafanya mikutano ya kwanza barani Afrika katika kipindi cha miaka 50

Mkuu wa Mfuko wa Fedha wa Kimataifa (IMF) Kristalina Georgieva ametoa wito kwa mataifa tajiri kutoa msaada zaidi kwa nchi zinazoendelea zenye madeni, wakati akifungua mikutano ya kwanza ya IMF na Benki ya Dunia kufanywa katika ardhi ya Bara la Afrika katika kipindi cha miaka 50.

"Kuleta mikutano barani Afrika tena, ni hatua muhimu sana kiishara na kimaana," amesema Georgieva katika mkutano na wanachama wa mashirika ya kiraia.

Amebainisha kuwa bara hilo linapambana na matatizo "yanayofanana sana" kama miaka 50 iliyopita, ikiwa ni pamoja na mfumuko wa bei na "machafuko ya kisiasa katika maeneo mengi".

"Nchi nyingi ziko chini ya mzigo wa madeni ambayo yanaweza kuzikandamiza na tunatumai sana kwamba mikutano hii itakuwa mahali pa kujenga uaminifu zaidi miongoni mwa mataifa. Sote tunahitajiana," amesisitiza mkuu huyo wa IMF.

Majadiliano ya muda wa juma moja yanayofanyika katika mji wa Marrakesh Kusini mwa Morocco ambayo yalianza jana Jumatatu, yanaendelea wakati IMF na Benki ya Dunia zinakabiliwa na wito wa kufanya mageuzi ili kuyapatia misaada mikubwa zaidi mataifa yaliyo katika hali hatarishi ya kukabiliana na umaskini na mabadiliko ya tabianchi.

Wakopeshaji wa kimataifa kwa kawaida huwa wanajumuika pamoja kupitia mkutano wa mawaziri wa fedha na magavana wa benki kuu nje ya makao makuu yao Washington kila baada ya miaka mitatu. Marrakesh ilipaswa kuandaa mkutano huo mnamo mwaka 2021, lakini uliahirishwa mara mbili kwa sababu ya janga la Covid-19.

 
Tetemeko kubwa la ardhi ambalo liliua karibu watu 3,000 katika eneo la kusini mwa Marrakesh mwezi uliopita lilitishia kuakhirishwa tena mkutano huo lakini serikali ya Morocco iliamua uendelee kufanyika.
 
IMF na Benki ya Dunia zilifanya mikutano yao barani Afrika kwa mara ya mwisho mwaka 1973, wakati Kenya ilipoandaa hafla hiyo, huku baadhi ya mataifa ya bara hilo yakiwa yangali yako chini ya tawala za kikoloni.../
 

 

Tags