Watu 30 waaga dunia katika ajali mbaya ya barabarani nchini Nigeria
Kwa akali watu 30 wamepoteza maisha kufuatia ajali mbaya ya barabarani iliyotokea usiku wa kuamkia leo kusini magharibi mwa Nigeria.
Msemaji wa Mamlaka ya Usalama Barabarani nchini humo, Bisi Kazeem amesema ajali hiyo ilitokea baada ya mabasi mawili ya abiria kugongana ana kwa ana katika barabara kuu ya Lagos-Ibadan.
Amesema makumi ya abiria wamejeruhiwa katika ajali hiyo na kwa sasa wanatibiwa katika Hospitali ya Adeoyo Yemetu mjini Ibadan.
Hii sio mara ya kwanza kwa ajali mbaya ya barabarani kufanyika katika nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika. Mwezi Mei mwaka huu, watu 26 walipoteza maisha katika ajali nyingine mbaya ya barabarani katika mji wa Lagos magharibi mwa Nigeria.
Kwa mujibu wa takwimimu rasmi za Mamlaka ya Usalama Barabarani nchini Nigeria, zaidi ya watu elfu 5 walipoteza maisha kutokana na ajali za barabarani nchini humo mwaka jana pekee.
Nchi ya Nigeria imekuwa ikikumbwa na visa vya ajali za barabarani kutokana na hali mbaya za magari, barabara pamoja na kutozingatiwa sheria za barabarani.