Rais na Waziri Mkuu wa zamani wa Tunisia kugombea kiti cha urais
Rais na Waziri Mkuu wa zamani wa Tunisia wametangaza kuwa watagombea kiti cha urais katika uchaguzi ujao nchini humo.
Moncef al Marzouq Rais wa zamani wa Tunisia na Hamadi Jebali aliyekuwa Waziri Mkuu wa nchi hiyo jana Jumanne walitangaza kuwa, watagombea kiti cha urais katika uchaguzi ujao. Mbali na Moncef al Marzouq na Hamadi Jebali ambao ni miongoni mwa shakhsia watajika ambao wametangaza kuwa watagombea kiti cha urais huko Tunisia, Mahdi Juma'a kutoka chama cha al-Badil naye pia atashiriki kwenye uchaguzi huo; huku wagombea wengine wakitarajiwa kuwa wa kujitegemea au kutoka katika vyama vingine ambavyo siyo mashuhuri.
Rais Mohamed Beji Caid Essebsi Rais wa Tunisia aliaga dunia tarehe 25 mwezi Julai mwaka huu; na sasa mchuano mpya unashuhudiwa huko Tunisia baina ya vyama mbalimbali vya siasa kwa ajili ya kuwania kiti cha urais.
Katiba ya Tunisia inasema kuwa, kila mgombea anapasa kukusanya saini kumi za ndio kutoka kwa wabunge kumi au raia elfu kumi wa Tunisia ili kuweza kujiandikisha kuwa mgombea wa kiti cha urais. Zoezi la kujiandikisha wagombea wa kiti cha uchaguzi Tunisia limeanza tangu Ijumaa iliyopita Agosti Pili katika makao makuu ya Tume Kuu ya Uchaguzi ya nchi hiyo.