Dikteta wa Tunisia afariki dunia ukimbizini Saudia
Vyombo vya habari vya Tunisia vimetangaza habari ya kufariki dunia dikteta wa zamani wa nchi hiyo, Zine El Abidine Ben Ali akiwa ukimbizini nchini Saudi Arabia
Kwa mujibu wa vyombo hivyo vya habari, Ben Ali amefariki dunia akiwa na umri wa miaka 83 baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Siku nne zilizopita, baadhi ya vyombo vya habari vya Kiarabu vilinukuu duru mbalimbali zikitangaza kwamba Ben Ali ameshafariki dunia, lakini habari hiyo haikuthibitishwa na watu wa familia ya dikteta huyo.
Ben Ali alikuwa kiongozi wa kwanza wa nchi za Kiarabu kupinduliwa katika mapinduzi ya wananchi mwaka 2011. Alikimbilia Saudi Arabia baada ya nchi za Magharibi kukataa kumpokea wakati alipotoroka nchi yake kukimbia hasira za wananchi licha ya kwamba alikuwa kibaraka mkubwa wa nchi za Magharibi. Hatimaye utawala wa kiimla wa Saudi Arabia ulimpokea na kubakia huko hadi kifo chake.
Saudi Arabia ilikataa kumkabidhi dikteta huyo kwa Tunisia licha mahakama ya kijeshi ya nchi hiyo kumuhukumu kifungo cha miaka 20 jela kwa kosa la kuua wapinzani wake wa kisiasa na licha ya Tunisia kuitaka rasmi Saudia imkabidhi diteta huyo.