Pande hasimu Libya zasaini makubaliano ya usitishaji vita
Pande zinazozozana Libya leo Ijumaa zimesaini makubaliano ya kusitisha vita chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa. Makubaliano hayo yamesaini huko Geneva nchini Uswisi
Stephanie Williams Mjumbe Maalumu wa Umoja wa Mataifa katika Masuala ya Libya ameashiria makubaliano hayo yaliyofikiiwa kati ya Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa ya Libya na kundi la Jeshi la Kitaifa la Libya linaloongozwa na kamanda Khalifa Haftar kwa ajili ya kusitisha vita nchini humo na kueleza matarajio kwamba yanaweza kuhitimisha matatizo yanayowakabili wananchi wa Libya.
Williams amesema kuwa makubaliano hayo yanaeleza kuwa: Wanajeshi wote wa nchi ajinabi wanapaswa kuondoka Libya katika kipindi cha miezi mitatu na kwamba makubaliano hayo yatarejesha usalama na amani nchini humo.
Libya ilitumbukia katika hali ya machafuko na ukosefu wa amani tangu mwaka 2011 baada ya kung'olewa madarakani dikteta wa nchi hiyo, Muammar Gaddafi, katika mapinduzi yaliyofanywa na wananchi na kufuatiwa na uingiliaji kati wa Marekani na baadhi ya nchi za Ulaya. Kwa sasa nchi inaongozwa na serikali mbili tofauti.