Rais wa Iran aelekea Uswisi na Austria kwa ziara rasmi
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i46505-rais_wa_iran_aelekea_uswisi_na_austria_kwa_ziara_rasmi
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo anaanza safari rasmi ya kuzitembelea nchi za Uswisi na Austria kufuatia mwaliko rasmi wa viongozi wa nchi hizo mbili za bara Ulaya.
(last modified 2023-11-27T12:14:11+00:00 )
Jul 02, 2018 02:32 UTC
  • Rais wa Iran aelekea Uswisi na Austria kwa ziara rasmi

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran leo anaanza safari rasmi ya kuzitembelea nchi za Uswisi na Austria kufuatia mwaliko rasmi wa viongozi wa nchi hizo mbili za bara Ulaya.

Kwa mujibu wa taarifa ya Parviz Ismaili, mkuu wa idara ya habari ya ofisi ya rais wa Iran, katika safari hiyo ya siku mbili, Rais Hassan Rouhani anaongoza ujumbe wa ngazi za juu wa kisiasa na kiuchumi. Kwa mujibu wa Ismaili, katika duru ya kwanza ya safari hiyo, Rais wa Iran ataitembelea Uswisi na kukutana na Rais Alain Berset wa nchi hiyo. Katika ziara hiyo, nchi mbili zitatiliana saini mikataba kadhaa ya ushirikiano katika nyuga za kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni.

Akiwa nchini Austria Rais wa Iran anatazamiwa kukutana na Kansela  Sebastian Kurz  wa nchi hiyo na kisha nchi mbili zitatiliana saini mapatano kadhaa ya ushirikiano.

Rais Hassan Rouhani (kulia) akizungumza na Waziri wa Mambo ya Nje wa Austria Sebastian Kurz alipotembelea Tehran Aprili 2014. Hivi sasa Kurz ni Kansela wa Austria

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la Austria. (APA), nchi hiyo imepuuza mashinikizo ya Marekani na ina azma ya kuimarisha uhusiano wake na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.

Gazeti la Der Standard la Ausria limesema katika safari ya Rais Rouhani, Kansela Kurz anatazamiwa kusisitiza kuwa nchi yake inaunga mkono mapatano ya nyuklia ya Iran yanayojulikana kama Mpango Kamili wa Pamoja wa Utekezwaji, JCPOA.