Vikosi vya Yemen vyatungua 'drone' ya Marekani
Vikosi vya Yemen vikishirikiana na wapiganaji wa harakati ya Ansarullah vimefanikiwa kutungua ndege isiyo na rubani ya Marekani iliyokuwa inapita katika anga ya mji mkuu Sana'a.
Kanali ya televisheni ya al-Masirah inayorusha matangazo yake kwa lugha ya Kiarabu imenukuu duru za kijeshi zikisema kuwa, vikosi vya Yemen vimetungua drone hiyo ya Marekani aina ya General Atomics MQ-9 Reaper inayofahamika kwa jingine kama Predator B.
Habari zaidi zinasema kuwa, drone hiyo ya upelelezi ya US ilikuwa inaruka katika wilaya ya Jeddar, kaskazini mwa Sana'a kabla ya kutunguliwa.
Mapema mwaka huu, watu kadhaa waliuawa nchini Yemen kufuatia hujuma ya drone za Marekani katika mkoa wa Bayda.
Mbali na Yemen, ndege zisizo na rubani za Marekani zimekuwa zikitumiwa kushambulia maeneo mbalimbali nchini Somalia, Afghanistan, Libya na Pakistan.