Mkuu wa Baraza Kuu la Mashia Lebanon: Israel inachezea moto
(last modified Sun, 25 Aug 2019 12:31:52 GMT )
Aug 25, 2019 12:31 UTC
  • Mkuu wa Baraza Kuu la Mashia Lebanon: Israel inachezea moto

Mkuu wa Baraza Kuu la Mashia nchini Lebanon amesema, kuendeleza utawala wa Kizayuni wa Israel uchokozi dhidi ya Lebanon na Syria ni kuchezea moto, ambao utapelekea kuteketezwa utawala huo.

Sheikh Abdulamir Qablan amelaani shambulio la ndege isiyo na rubani lililofanywa na utawala wa Kizayuni wa Israel nchini Lebanon hii leo na kusisitiza kwamba, uvamizi na uchokozi huo, ambao umefanywa katika sherehe za kuadhimisha kukombolewa Juroud Arsal na ushindi mkubwa wa jeshi la Syria dhidi ya magaidi unaonyesha kuwa ugaidi wa Kizayuni na Kitakfiri umedhamiria kuudhuru mhimili wa Muqawama.

Kukombolewa miinuko ya mashariki ya Lebanon ya Juroud Arsal na kutokomezwa kikamilifu makundi ya kigaidi ya Daesh na An-Nusrah katika maeneo hayo mnamo Agosti 26 mwaka 2017, ni maarufu nchini Lebanon kama siku ya Idi ya Ukombozi wa Pili, ambalo ni tukio lenye muhimu katika historia ya nchi hiyo, sawa na wa kukombolewa eneo la kusini mwa nchi hiyo mnamo mwaka 2000 baada ya kukaliwa kwa mabavu kwa miaka kadhaa na utawala haramu wa Israel.

Wanamuqawama wa Hizbullah walioyakomboa maeneo ya ardhi ya Lebanon kutoka kwenye makucha ya Wazayuni na magaidi wakufurishaji

Wakati huohuo, Waziri Mkuu wa Lebanon Saad Hariri amesema, kuingia ndege zisizo na rubani za utawala wa Kizayuni kusini mwa mji mkuu Beirut ni ukiukaji wa wazi wa mamlaka ya kujitawala Lebanon pamoja na azimio nambari 1701 na kuongeza kuwa, hatua hiyo ni tishio kwa uthabiti wa eneo na inalenga kuzusha hali ya wasiwasi.

Azimio nambari 1701 lilipitishwa Agosti 11 mwaka 2006 na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa  kwa ajili ya kuhitimisha vita kati ya Hizbullah ya Lebanon na utawala wa Kizayuni wa Israel.

Vyombo vya habari vilitangaza mapema leo kuwa ndege mbili zisizo na rubani (droni) za utawala wa Kizayuni zimedondoka katika eneo la Dhahiyah, kusini mwa mji mkuu wa Lebanon, Beirut.../

Tags