Israel yabomoa makumi ya nyumba za Wapalestina Ukingo wa Magharibi
Jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel limebomoa madazeni ya nyumba za Wapalestina katika eneo la Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, huko Palestina inayokaliwa kwa mabavu.
Duru za habari zinaeleza kuwa, idadi kubwa ya wananchi wa Palestina wameachwa bila makazi kutokana na bomoa bomoa hiyo ya utawala wa Kizayuni wa Israel katika eneo la al-Muarrajat, mashariki mwa mji wa Ramallah katika Ukingo wa Magharibi.
Mmoja wa Wapalestina waliobomolewa nyumba zao, Avde al-Kabne ameliambia shirika la habari la Anadolu kuwa, ubomozi huo wa wanajeshi wa utawala haramu wa Israel umewaacha Wapalestina zaidi ya 25 aghalabu yao wakiwa ni watoto wadogo bila makazi.
Amesema kitendo hicho hakijawaacha na chochote isipokuwa nguo walizozivaa; na kwamba askari hao wa Kizayuni mbali na kubomoa nyumba zao, lakini pia wanaiba milki na vitu vyao.
Weledi wa mambo wanasema kuwa, utawala wa Kizayuni unabomoa nyumba za wananchi wa Palestinana hivyo inatekeleza kivitendo mpango wake wa kuikalia kwa mabavu sehemu kubwa ya ardhi ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.
Sheria za kimataifa zinautambua mji wa Quds Mashariki na Ukingo wa Magharibi kama maeneo ya Wapalestina yanayokaliwa kwa mabavu.