Mkuu wa mtandao wa fedha wa shirika la ujasusi la Israel Mossad atiwa mbaroni nchini Uturuki
(last modified Wed, 04 Sep 2024 02:38:42 GMT )
Sep 04, 2024 02:38 UTC
  • Mkuu wa mtandao wa fedha wa shirika la ujasusi la Israel Mossad atiwa mbaroni nchini Uturuki

Polisi wa Istanbul wamemtia mbaroni Liridon Rexhepi, ambaye Shirika la Taifa la Intelijensia la Uturuki (MIT) limemtambua kama Mkuu wa Mtandao wa Fedha wa shirika la ujasusi la utawala wa Kizayuni wa Israel Mossad ndani ya nchi hiyo. Hayo ni kwa mujibu wa ripoti zilizotolewa jana Jumanne na duru za usalama za Uturuki.

Kwa mujibu wa duru hizo, Rexhepi alikuwa akisimamia shughuli za kifedha za Mossad nchini Uturuki, ambapo imefichuliwa kuwa, kwa maelekezo ya shirika hilo la ujasusi la Israel, jasusi huyo aliendesha operesheni za uchunguzi kwa kutumia ndege zisizo na rubani na operesheni za kisaikolojia dhidi ya wanasiasa wa Palestina.
 
Rexhepi amegunduliwa kuwa alihamisha fedha kuwapatia maajenti wa ugani wa Mossad huko Uturuki ambao walikuwa wakikusanya taarifa za kijasusi kuhusu Syria.

Taarifa zinaeleza kuwa, shughuli mbalimbali za Rexhepi, ikiwa ni pamoja na za uhamishaji fedha wenye kutia shaka kupitia akaunti zake, zilianza kufuatiliwa na MIT, ambapo uchunguzi ulibaini kuwa alihamisha kiasi kikubwa cha pesa kupitia wakala wa Western Union kuwapelekea maajenti wa ugani wa Mossad walioko Uturuki. Shughuli za jasusi huyo wa Mossad zilianza kufuatiliwa tangu alipoingia nchini Uturuki Agosti 25.

 
Rexhepi, ambaye alitiwa nguvuni Agosti 30 na maafisa wa MIT wakishirikiana na Polisi alikiri kuhamisha fedha hizo.
Kabla ya hapo, Polisi ya Uturuki ilishawatia nguvuni maajenti kadhaa wa Mossad nchini humo. 
 
Operesheni za Shirika la Taifa la Intelijensia la Uturuki MIT zimefichua pia kuwa Mossad ilifadhili maajenti wake wa ugani nchini humo kupitia nchi za Ulaya Mashariki, hususan Kosovo.
 
Uchunguzi uliofanywa umeonyesha kuwa fedha kutoka Kosovo zilihamishiwa kwa maajenti wa Syria kupitia wakala wa Western Union na sarafu za kripto.../

 

 

Tags