Sep 07, 2024 10:59 UTC
  • Baada ya jela zake kujaa, Uingereza inafikiria kuwahamishia wafungwa wake Estonia

Gazeti la Telegraph limeripoti kuwa, Serikali ya Uingereza inafikiria kukodi nafasi katika magereza ya Estonia kutokana na jela zake kufurika wafungwa.

Kwa mujibu wa toleo la Ijumaa la gazeti hilo, Wizara ya Sheria ya Uingereza inatathmini shauri la kuwahimisha baadhi ya wahalifu wa nchi hiyo wakatumikie vifungo vyao katika magereza ya Estonia ili kukabiliana na msongamano wa wafungwa katika jela zake.

Estonia, nchi ya eneo la Baltic ilitangaza mwishoni mwa mwezi uliopita kwamba inaweza kukodisha nafasi kwenye magereza yake na kupokea wahalifu kutoka nchi zingine ili kuongeza mapato kwa ajili ya bajeti ya serikali.

Kulingana na ripoti ya Telegraph ambayo imenukuu vyanzo vya serikali ya Uingereza, suluhisho hilo lenye utata limewekwa mezani kujadiliwa kutokana na hali mbaya katika jela za nchi hiyo.

Wafungwa wamejaa katikka Jela za Uingereza

Wizara ya Sheria imesema inachunguza "machaguo yote yanayoyumkinika" ili kuongeza uwezo wa kushughulikia wafungwa kwa sababu magereza nchini humo "yanakaribia kuporomoka."

Idadi ya magereza ya Uingereza inatarajiwa kuongezeka kutoka karibu jela 89,000 hadi kati ya 93,100 na 106,300 ifikapo Machi 2027. Magereza ya wanaume nchini Uingereza na Wales yalikaribia kukosa seli za kuwekea wafungwa mwezi uliopita, baada ya kubakiwa na nafasi 83 tu.

Kiwango cha chini cha uhalifu nchini Estonia kinamaanisha kuwa nusu ya magereza yake ni matupu na serikali ya Tallinn inatarajia kwamba mpango wake wa kukodisha jela unaweza kuipatia nchi hiyo kwa mwaka yuro milioni 30 ($ milioni 33) inazohitaji.../

Tags