UN yatahadharisha kuhusu maafa ya mabomu ya kutegwa ardhini duniani
Umoja wa Mataifa umetangaza kuwa, watu wasiopungua 10 hufariki dunia kila siku kutokana na kulipuka kwa mabomu ya kutengwa ardhi katika maeneo mbalimbali duniani.
Bruno Donat ambaye ni mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Operesheni dhidi ya Mabomu ya Kutegwa Ardhini (UNMAS) amesema kuwa, asilimia 40 ya wahanga wa milipuko ya mabomu hayo duniani ni watotro wadogo. Donat ameongeza kuwa, katika mwaka uliopita wa 2015 karibu kilomita mraba 64 ambazo ni sawa na viwanja elfu 16 vya mpira wa miguu, zilisafishwa na mabomu ya kutegwa ardhini.
Nchi nne za Afrika ambazo ni Misri, Angola, Msumbiji na Somalia zipo katika orodha ya nchi kumi zinazoongoza duniani kwa kuwa na idadi kubwa zaidi ya mabomu yaliyotengwa ardhini.
Siku ya leo ya tarehe 4 Aprili imepewa jina la siku ya kimataifa ya kutanabahisha watu kuhusu mabomu ya kutengwa ardhini na ushirikiano katika operesheni ya kutegua mabomu hayo. Lengo la hatua hiyo ni kuwaelimisha watu kuhusu hatari ya aina hiyo ya mabomu na njia za kukabiliana nayo.