Majanga yazidi kumwandama Trump, Kongresi kuchunguza uhalifu wa makampuni yake
-
Donald Trump
Mbunge wa chama cha Democratic katika Kongresi ya Marekani amesema kuwa ataanzisha uchunguzi kuhusu tuhuma za kuhusika taasisi na makampuni ya Rais wa nchi hiyo Donald Trump katika uhalifu wa utakatishaji wa fedha chafu na kuhusu uhusiano wake na Saudi Arabia.
Eric Swalwell ametoa kauli hiyo baada ya Rashida Tlaib ambaye ni mmoja kati ya wabunge wawili wa kwanza kabisa wa kike Waislamu nchini Marekani kutoa wito wa kufunguliwa mashtaka dhidi ya Donald Trump akimtaja kuwa ni tishio kwa demokrasia ya Marekani.
Eric Swalwell ambaye ni miongoni mwa wabunge wenye satua na ushawishi mkubwa wa chama cha Democratic amezungumzia pia uhusiano wa Taasisi ya Trump na Saudi Arabia na kuashiria mamia ya vyumba vilivyochukuliwa na maafisa wa utawala wa Saudia katika hoteli mpya ya kiongozi huyo wa Marekani mjini Washington baada ya kuchaguliwa kwake kuwa Rais wa Marekani na vilevile kuhusu kuwakingia kifua watawala wa Riyadh waliohusika na mauaji ya mkosoaji wa serikali ya nchi hiyo, Jamal Khashoggi.
Rais Donald Trump wa Marekani anakabiliwa na wimbi kubwa la ukosoaji la wabunge wa nchi hiyo hususan baada ya Kongresi kudhibitiwa na chama cha Domocratic.
Donald Trump anakabiliwa na changamoto nyingi za kisheria na mashtaka mengi yakiwemo ya faili la uhalifu uliofanyika katika uchaguzi wa rais wa Marekani mwaka 2016 na kwa msingi huo baadhi ya mafisa wa sasa na wa zamani wa serikali ya nchi hiyo wanasema kuna uwezekano mkubwa akalazimika kujiuzulu mwaka huu wa 2019 mkabala wa kupewa dhamana ya kutochukuliwa hatua yoyote.