Jun 05, 2020 17:09 UTC
  • Ugiriki: Tumejiweka tayari kupambana kijeshi na Uturuki

Waziri wa Ulinzi wa Ugiriki amesema kuwa nchi yake imejiweka tayari kwa ajili ya kukabiliana kijeshi na Uturuki kwa ajili ya kulinda haki yake ya kujitawala.

Nikos Panagiotopoulos ameyasema hayo leo na kuongeza kwamba iwapo harakati za Uturuki zitaendelea katika maji ya Mediterrania, basi nchi yake haitakuwa na budi ispokuwa kukabiliana kijeshi na jirani yake huyo kwani imejiandaa kwa ajili ya kutetea haki yake ya kujitawala. Akibainisha kwamba mienendo ya hivi karibuni ya Uturuki imekuwa hatari, Waziri wa Ulinzi wa Ugiriki ameongeza kwamba jeshi la nchi hiyo linafuatilia kwa karibu sana harakati zote za Uturuki.

Viongozi wa Ugiriki na Uturuki ambao wamekuwa mahasimu wakubwa

Jumatano iliyopita, Waziri Mkuu wa Ugiriki sambamba na kutuma barua kwenda kwa viongozi wa nchi za Ulaya, alionya kwamba harakati za Uturuki dhidi ya nchi yake zitapelekea kuibuka mgogoro mkubwa kati ya nchi mbili hizo. Uturuki na Ugiriki zinazozania suala la kuchimba mafuta katika kisiwa kilichopo katika maji ya bahari ya Mediterrania. Aidha Alkhamisi iliyopita, Rais Recep Tayyip Erdoğan wa Uturuki na akizungumza na waandishi wa habari akiwa pamoja na Fayez al-Sarraj, Rais wa Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa nchini Libya alisema kuwa, nchi mbili zitapanua shughuli zao za kuchimba mafuta na gesi katika maji ya Mediterrania.

Tags