Huenda usajili wa wapiga kura DRC ukaakhirishwa, kisa machafuko
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i26408-huenda_usajili_wa_wapiga_kura_drc_ukaakhirishwa_kisa_machafuko
Kanisa Katoliki na Tume ya Uchaguzi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zimetahadharisha kuwa, yumkini zoezi la kuwasajili wapiga kura likakosa kufanyika kutoka na kushtadi machafuko na mapigano nchini humo.
(last modified 2025-12-16T11:48:21+00:00 )
Mar 15, 2017 07:04 UTC
  • Huenda usajili wa wapiga kura DRC ukaakhirishwa, kisa machafuko

Kanisa Katoliki na Tume ya Uchaguzi katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo zimetahadharisha kuwa, yumkini zoezi la kuwasajili wapiga kura likakosa kufanyika kutoka na kushtadi machafuko na mapigano nchini humo.

Corneille Nangaa, Mwenyekiti wa Tume yaTaifa ya Uchaguzi nchini humo CENI amebainisha kuwa, ofisi nne za tume hiyo ziliteketezwa moto na watu wasiojulikana katika machafuko ya hivi karibuni eneo la Kasai.

Mwezi uliopita, Richard Ngoie Kitangala, Gavana wa mkoa wa Tanganyika mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo alisema kuwa, watu 150 wameuawa hadi sasa, 200 wamejeruhiwa, shule 400 zimebomolewa na vijiji 422 kuchomwa moto tangu kuanza tena mapigano katika mkoa huo.

Maafisa usalama wakikabiliana na waandamanaji Kinshasa

Askofu Félicien Mwanama wa Kanisa Katoliki Kongo DR ameonya kuwa, kuna wimbi la mauaji ya raia yanayofanywa na jeshi la nchi hiyo katika mikoa ya Kasai, Kasai ya Kati, Kasasi Oriental na Lomami, na machafuko haya huenda yakawa sabibu ya kutofanyika uchaguzi unaotazamiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu.

Siku chache ziliopita, maafisa wawili wa Umoja wa Mataifa raia wa Marekani na Sweden walitekwa nyara katika mkoa wa Kasai katikati ya Kongo DR, wiki moja baada ya watu wanne kuuawa katika mapigano kati ya polisi na kundi moja linaloipinga serikali kati mji mkuu Kinshasa.

Kushindwa jeshi la Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo kuyaangamiza makundi ya wanamgambo nchini humo, kumesababisha kuenea hali ya mchafukoge na ukosefu wa amani nchini humo.