Feb 17, 2018 08:14 UTC
  • Watu 18 wauawa katika shambulizi la kigaidi Maiduguri

Magaidi watatu waliokuwa wamejifunga mabomu wameua watu wasiopungua 18 katika mji wa Maiduguri ulioko kaskazini mashariki mwa Nigeria ambao ni makao makuu ya jimbo la Borno lililoathiriwa zaidi na mashambulizi ya kundi la kigaidi la Boko Haram.

Kamishna wa Polisi ya jimbo la Borno, Damian Chukwu amesema shambulizi hilo limefanyika katika soko la samaki lililoko umbali wa kilomita 20 kutoka katikati ya mji wa Maiduguri.

Chukwu ameongeza kuwa, raia 18 na magaidi watatu wameaga dunia katika shambulizi hilo ambalo limejeruhi watu wengine 22.

Mashambulizi ya kujilipua kwa mabomu yanaendelea kushuhudiwa nchini Nigeria licha ya serikali na jeshi la nchi hiyo kudai kwamba limeliangamiza kundi la kigaidi la Boko Haram tangu mwaka 2016. 

Rais wa sasa wa Nigeria, Muhammadu Buhari aliyeshika madaraka ya nchi mwaka 2015 aliahidi kuboresha usalama katika maeneo ya kaskazini mwa nchi hiyo na kuliangamiza kabisa kundi la Boko Haram.

Tags