Jun 05, 2024 07:28 UTC
  • Iran, China na Russia zazitaka nchi za Magharibi zianze tena kutekeleza makubaliano ya nyuklia

Iran, China na Russia zimesisitiza kuwa, vifungu vya mkataba wa nyuklia wa JCPOA vingali vina itibari na kuzishauri nchi za Magharibi ambazo zimekwamisha utekelezaji wa mapatano hayo kwa kutochukua hatua na kukhalifu kutekeleza ahadi na majukumu yao, zionyeshe utashi wa kisiasa na kuchukua hatua zinazohitajika ili kuanza kutekeleza tena makubaliano hayo.

Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa na IRNA mapema leo, katika taarifa ya pamoja ambayo imewasilishwa kwa mara ya kwanza na nchi tatu za Iran, China na Russia katika mkutano wa robo ya mwaka wa Bodi ya Magavana wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki, IAEA imeelezwa na nchi hizo: "nchi zetu zimekuwa waungaji mkono wa kudumu na wa dhati wa JCPOA".
 
Taarifa hiyo iliyowasilishwa na Mikhail Ulyanov, balozi na mwakilishi wa kudumu wa Russia katika mashirika ya kimataifa yaliyoko Vienna, imeongeza kuwa: "tangu mwaka 2018, wakati Marekani ilipojiondoa peke yake na kinyume cha sheria katika makubaliano haya huku uwekaji vikwazo vya upande mmoja na vilivyo kinyume cha sheria na utekelezaji wa sera ya mashinikizo ya juu kabisa dhidi ya Iran ukiwa ni  nukta ya mabadiliko makubwa katika makubaliano haya, uungaji mkono wetu kwa JCPOA haujabadilika".
Mikhail Ulyanov

Iran, China na Russia zimesisitiza kuwa, kwa muda wote huo hazijaacha kufanya kila juhudi ili kuyarejesha makubaliano ya JCPOA na kukumbusha kuwa kutokana na matokeo yaliyopatikana kwenye duru nane za mazungumzo ya Vienna, zinatangaza utayarifu wao wa kufikia tena makubaliano ya kuanza kutekeleza JCPOA kulingana na matini ya Agosti 2022.

 
Hii ni katika hali ambayo, kwa mujibu wa taarifa hiyo, "washiriki wengine wa JCPOA - yaani Ufaransa, Ujerumani na Uingereza - pamoja na Marekani", licha ya ahadi walizotoa, wamechagua mchakato mwingine na kulipuuza kwa sababu za kisiasa lengo letu la pamoja la kuanzisha tena utekelezaji wa JCPOA".
 

Mazungumzo ya kuanza kutekeleza tena JCPOA yalifanyika kuanzia tarehe 27 Disemba 2021 mjini Vienna katika duru nane kwa kuhudhuriwa na wawakilishi wa Kundi la 4+1, Umoja wa Ulaya na Iran.

Ujumbe wa Marekani nao pia ulishiriki kwenye mazungumzo hayo kwa njia isiyo ya moja kwa moja, lakini mazungumzo hayo yaliishia kwenye mkwamo kutokana na sababu kadhaa ikiwa ni pamoja na migongano katika muamala, kuchelewa kuchukua uamuzi, kujivutia zaidi maslahi yake Marekani na kuibua matakwa mengine mapya.../

Tags