Mar 14, 2024 03:23 UTC
  • Sayyid Nasrullah: Jeshi la Israel limechoka, litashindwa na muqawama

Katibu Mkuu wa Harakati ya Hizbullah ya Lebanon amesema jeshi la utawala wa Kizayuni wa Israel linaloendeleza mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina wasio na ulinzi wa Ukanda wa Gaza limechoka, na hakuna shaka kwamba litashindwa na kambi ya muqawama hata likiamua kuuvamia mji wa Rafah.

Sayyid Hassan Nasrullah alisema hayo katika hotuba yake ya televisheni iliyotangazwa moja kwa moja kutoka mji mkuu wa Lebanon, Beirut jana Jumatano, kwa mnasaba wa kuwadia mwezi mtukufu wa Ramadhani na kuongeza kuwa, "Jeshi la Israel hii leo ni chovu katika nyanja zote. Wataalamu waandamizi wa adui wanadiriki kushindwa huko na vipigo vya kistratajia (dhidi ya Israel)."

Ameleeza bayana kuwa: Kusimama kidete, kukabiliana kushujaa na muqawama wa (Wapalestina wa) Gaza, ni matukio ambayo yanakaribiana na muujiza, na yote haya yametokana na utamaduni wa Qurani na dalili zake tukufu kwa ulimwengu wote.

Sayyid Nasrullah amesema idadi ya askari wa Kizayuni waliouawa katika medani ya vita ni kubwa zaidi ya ile inayotangazwa na adui na kuongeza kuwa, "Sisi tunatangaza hadharani mashahidi wetu, lakini maadui wanaficha watu wao walioangamizwa, jambo hili lina taathira kwa jeshi la Israel." 

Aidha Katibu Mkuu wa Hizbullah ya Lebanon ameilaumu vikali Washington kwa uungaji mkono wake usiosita kwa Israel katika vita vyake vya mauaji ya kimbari huko Gaza na kusema, "Serikali ya Marekani ni ya kipumbavu, ni vyema ikisimamisha vita dhidi ya Gaza. (Rais wa Marekani Joe) Biden iwapo atataka atasimamisha uvamizi wa Wazayuni dhidi ya Gaza ndani ya sekunde chache."

Mrengo wa muqawama unaomkosesha usingizi adui Mzayuni

Huku akisisitiza kuwa lengo la utawala wa Israel la kuua raia ni kushinikiza kuvunjwa muqawama, Nasrullah amesema mrengo wa muqawama utaendelea kuisaidia na kuihami Gaza kupitia msaada wa kijeshi na kifedha, lakini pia kupitia dua na maombi.

Kadhalika Sayyid Hassan Nasrullah amesisitiza kuwa: Kinachofanyika leo hasa huko Gaza kinapasa kutoa funzo na ibra kwa mataifa ya dunia, na tunapaswa kutambua mafanikio makubwa ya Operesheni ya Kimbunga cha al-Aqsa iliyoanzishwa na HAMAS Oktoba 7.

Ameongeza kuwa, "utawala wa Kizayuni utashindwa tu hata kama (Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin) Netanyahu ataivamia Rafah. Kamwe hawawezi kuisambaratisha HAMAS au muqawama."

Tags