Makundi yanayoipinga serikali ya Syria yanaendesha propaganda dhidi yake
Kundi moja kwa jina la "Kofia Nyeupe" limetoa mkanda bandia wa video kuhusu shambulio la kemikali lililotekelezwa hivi karibuni katika mji wa Khan Sheikhoun nchini Syria.
Jumuiya ya Madaktari kwa ajili ya Haki za Binadamu ya Sweden imeutaja mkanda huo wa video uliotolewa na kundi hilo la Kofia Nyeupe huko Syria kuhusu shambulio la kemikali lililotekelezwa hivi karibuni huko Khan Sheikhoun kuwa ni bandia. Jumuiya hiyo ya Sweden imetangaza kuwa picha zilizoonyeshwa na kundi hilo ambazo zinawaonyesha watoto walioathiriwa na shambulio la kemikali lililotekelezwa hivi karibuni katika eneo la Khan Sheikhoun nchini Syria ni propaganda dhidi ya serikali ya Syria. Marekani na baadhi ya nchi za Magharibi zinazoipinga serikali ya Syria ambazo hadi sasa zimechochea kuasisiwa makundi ya kigaidi kwa kuwaunga mkono wapinzani wa Bashar al Assad, zimeituhumu Damascus kuwa imehusika na shambulio hilo la kemikali la Jumanne iliyopita kusini mwa mji wa Idlib huko Syria.
Hii ni katika hali ambayo serikali ya Syria mwaka 2014 ilikabidhi ghala lake la silaha za kemikali kwa wawakilishi wa Umoja wa Mataifa na Shirika Linalopiga Marufuku Silaha za Kemikali Duniani. Serikali ya Syria pia ilituma barua zaidi ya 90 kwa Umoja wa Mataifa zilizobainisha wazi na kwa kina kuhusu namna magaidi wanavyotumia silaha na mada za kemikali dhidi ya wananchi madhulumu wa Syria. Watu zaidi ya 100 wameuawa na wengine karibu ya 400 kujeruhiwa katika shambulio la kemikali la Jumanne iliyopita katika eneo la Khan Sheikhoun kusini mwa mji wa Idlib nchini Syria.