Khatibzadeh: Iran inachukua maamuzi kwa mujibu wa nyenendo za Marekani
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inachukua maamuzi kwa mujibu wa nyenendo na si kwa mujibu wa jumbe zisizo wazi za Marekani katika mazungumzo ya Vienna.
Akizungumza leo katika mkutano wa kila wiki na waandishi wa habari hapa Tehran akibainisha juu ya misimamo ya Iran kuhusu mazungumzo ya moja kwa moja na Marekani, Saeed Khatibzadeh amesema: Hadi sasa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imethibitisha wazi hatua zake na kwamba Tehran inachukua maamuzi kwa mujibu wa nyenendo za Marekani na si kwa mujibu wa jumbe zisizo wazi au bila ya kujua hatimaye nini kitatokea.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran ameendelea kubainisha kuwa, nchi wanachama katika mapatano ya JCPOA zinajua wazi kwamba Marekani imejitoa kwenye mapatano hayo na inataka kurejea; wajibu ambao inapasa kuukubali wazi mbele ya Iran na kwa nchi za kundi la 4+1.
Khatibzadeh amesisitiza kuwa: Hadi kufikia sasa hakujashuhudiwa mabadliko yoyote katika vitendo na hatua za Marekani bali nchi hiyo imeendeleza mashinikizo yake ya kiwango cha juu dhidi ya wananchi wa Iran. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran wakati huo huo ameashiria safari ya karibuni hapa Tehran ya Rafael Grossi Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Kimataifa wa Nishati ya Atomiki (IAEA) na mapatano yaliyofikiwa kati ya pande mbili na kuongeza kuwa, ziara hiyo imefanyika katika fremu ya masuala ya kiufundi ambayo yalikuwa utangulizi wa mazungumzo ya Vienna.
Saeed Khatibzadeh amesema: Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imejibu maswali ya wakala wa IAEA lakini ilipasa kujibu maswali hayo kwa mara nyingine tena katika fremu ya kiufundi na katika muda muafaka.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran aidha amesisitiza kuwa, kuna uhusiano wa moja kwa moja kati ya kusitishwa hoja za kiufundi za wakala wa IAEA na mapatano yanayofikiwa huko Vienna.