Mar 28, 2024 10:09 UTC
  • CAIR: UN ichunguze jeshi la Israel lilivyowaua Wapalestina bila sababu na kuzifukia maiti zao

Baraza la Mahusiano ya Kiislamu Marekani [CAIR] limetoa wito kwa Umoja wa Mataifa kuchunguza video inayoonyesha wanajeshi wa utawala wa Kizayuni wa Israel wakiwapiga risasi bila sababuu Wapalestina wawili wanaoonekana kuwa hawana silaha kisha kuzifukia maiti zao kwa buldoza.

Mkurugenzi wa Taifa wa Mawasiliano wa CAIR Ibrahim Hooper ameeleza katika taarifa: "uhalifu huu mbaya wa kivita na uhalifu mwingine kama huo unaofanywa kila siku na serikali ya Israel mfanyamauaji ya kimbari lazima uchunguzwe na Umoja wa Mataifa kama sehemu ya mauaji ya kimbari yanayoendelea, uangamizaji wa kizazi na kuwaweka na njaa kwa nguvu watu wa Palestina kwa ushirikiano na utawala wa Biden".
 
Msemaji wa CAIR ameongezea kwa kusema: "makundi ya serikali ya mrengo mkali wa kulia wa Israel yanaonekana yakiwaua Wapalestina kwa makusudi na kisha kuifanya miili yao kama takataka. Mauaji haya ya kimbari lazima yakomeshwe, si kusamehewa au kuungwa mkono kwa silaha na maneno".
Ibrahim Hooper

Picha za video zilizonaswa na televisheni ya Al Jazeera ya Qatar zinaonyesha wanaume wawili wa Kipalestina wasio na silaha, mmoja akipunga hewani kipande cha kitambaa cheupe mara kwa mara kuashiria kujisalimisha, kabla ya askari katili wa jeshi la kigaidi la utawala wa Kizayuni wa Israel kuwapiga risasi na kisha kuzifukia maiti zao kwenye kifusi kwa kutumia tingatinga karibu na mji wa Ghaza.

Harakati ya Muqawama wa Kiislamu ya Palestina HAMAS imelaani vikali mauaji hayo, ikisema "ni ushahidi zaidi unaoonyesha ukubwa wa ufashisti, jinai na uhalifu unaotawala tabia na khulka ya Wazayuni".

Naye Profesa Richard Falk, ripota maalum wa zamani wa Umoja wa Mataifa kuhusu hali ya haki za binadamu huko Palestina amesema, ufyatuaji risasi huo uliofanywa na askari wa Kizayuni ni "uthibitisho wa wazi wa kuendelezwa ukatili wa Israel huko Ghaza" na ambao umekuwa ni kama "jambo la kila siku".../

Tags