Mar 29, 2024 07:24 UTC
  • Wapalestina: Gati ya muda inayotaka kujenga Marekani Ghaza ni

Wapalestina wanaielezea gati ya muda inayojengwa na Marekani kwenye pwani ya mji wa Ghaza kuwa ni "bandari ya uvamizi na ukaliaji ardhi kwa mabavu".

Mchambuzi wa kisiasa wa Palestina Usama Abdulhadi ameshutumu Marekani na utawala haramu wa Israel kwa kutokuwa na nia njema kuhusu mradi huo.
 
Abdulhadi amesema: "kama wangekuwa na nia njema malori na mabuldoza makubwa yanayoingia Ghaza kujenga bandari yangechukua hatua kuokoa maelfu ya majeruhi wanaoendelea kuvuja damu hadi kufa chini ya vifusi vya nyumba zilizoharibiwa na utawala ghasibu wa Israel".
 
Mchambuzi huyo wa Kipalestina ametahadharisha kwa kusema: "gati hii itajengwa ili kuimarisha mamlaka vamizi ya Israel kwenye pwani ya Ghaza, kukifanya Kivuko cha Mpakani cha Rafah kisifanye kazi, kuhitimisha mamlaka ya Wapalestina na kuhamasisha na kuchochea uhajiri wa watu wa Ghaza".
 
Halikadhalika, Abdulhadi amesema Marekani na Israel zinataka kudhibiti sehemu ya pwani ya Ghaza kwa kisingizio cha kujenga gati, kuwezesha uingizaji misaada ya kibinadamu na kuzuia harakati ya Hamas kudhibiti eneo hilo.
 
"Hii ni bandari ya uvamizi na kukalia ardhi kimabavu, inayoruhusu wanajeshi wa Marekani kuingia kwenye mipaka ya Ghaza", ameeleza bayana mchambuzi huyo wa Kipalestina.
Joe Biden

Mnamo tarehe 7 Machi, Rais Joe Biden wa Marekani alitangaza kwamba amelikabidhi jeshi la Marekani jukumu la kujenga gati ya muda karibu na Ghaza kwa ajili ya kufikisha misaada ya kibinadamu inayohitajika sana, huku Israel ikiendelea kuruhusu chembe ndogo tu ya misaada kuingizwa katika eneo hilo kupitia nchi kavu.

Wizara ya Ulinzi ya Marekani Pentagon ilitangaza kuwa ujenzi wa gati hiyo ya muda unaweza kuchukua hadi siku 60, na baada ya hapo milo milioni mbili kwa siku itaweza kutolewa kwa ajili ya Wapalestina Ghaza.

Maombi ya Wapalestina ya kupatiwa vifaa vya kuondoa vifusi vya nyumba zilizopigwa mabomu katika miezi kadhaa ya mashambulizi ya Israel, kuopoa miili ya marehemu, na kusaidia waliojeruhiwa hayajajibiwa kwa muda wote wa kipindi cha miezi sita iliyopita.

Hata hivyo, katika wiki za hivi karibuni, kwa msaada wa Marekani, mabuldoza na malori mengi yaliyotumwa na Israel kwenye mpaka wa Ghaza yamekuwa yakisafirisha maelfu ya tani za vifusi kutoka kwenye nyumba zilizobomolewa huko Ghaza vikiwa na viungo vya miili ya watu hadi kwenye pwanii ya eneo hilo ili kutumika katika ujenzi wa gati mpya.../

 

 

 

Tags