Mwanamke mweusi mjamzito auawa kwa kupigwa risasi na askari polisi Marekani
(last modified Sat, 02 Sep 2023 06:38:04 GMT )
Sep 02, 2023 06:38 UTC
  • Mwanamke mweusi mjamzito auawa kwa kupigwa risasi na askari polisi Marekani

Polisi katika jimbo la Ohio nchini Marekani wametoa taswira ya filamu ya kamera zinazovaliwa na askari polisi inayoonyesha mwanamke mweusi mjamzito aitwaye Ta’Kiya Young akipigwa risasi, jambo ambalo limeibua taharuki na hasira ya umma huku kukitolewa wito mpya wa kukomeshwa ukatili mbaya unaofanywa na polisi wa nchi hiyo.

Filamu hiyo iliyotolewa Ijumaa imeonyesha mauaji ya kijana huyo mwenye umri wa miaka 21 katika maegesho ya duka la mbogamboga katika Mji wa Blendon, kitongoji cha mji mkuu wa jimbo la Ohio, Columbus, Agosti 24. Mamlaka husika imesema mtoto aliyekuwa tumboni wa Young hakunusurika kupigwa risasi.

Mkuu wa Polisi wa Mji wa Blendon John Belford ametaja tukio hilo kama "janga" lililotokea wakati polisi walipojaribu kumzuia Young baada ya kutuhumiwa kuwa aliiba dukani.

Lakini familia ya Young imeyaelezea mauaji hayo kuwa "yanayoweza kuepukika", ya "matumizi mabaya na makubwa ya nguvu na mamlaka" na "kitendo kilichotokana na chuki".

Maandamano ya kulalamikia mauaji ya kibaguzi yanayofanywa na Polisi ya Marekani dhidi ya watu weusi

Famila hiyo ya mwanamke huyo mjamzito imeendelea kueleza katika taarifa kama ilivyoripotiwa kama ilivyoripotiwa na gazeti la Columbus Dispatch kwamba, tukio lake linavuka kiwango cha ukiukaji wa wazi zaidi wa uchukuaji hatua kisheria. "Baada ya kuona picha za video za kifo chake, hiki ni kitendo cha uhalifu", imeongezea taarifa hiyo.

Ufyatuaji risasi huo ulitokea wakati polisi walipojaribu kusimamisha gari ya Young baada ya kutuhumiwa kuwa aliiba dukani.

 Familia ya mwanamke huyo imetangaza kuwa binti yao Young ambaye ana watoto wengine wawili alitarajiwa kujifungua mtoto wake huyo baada ya miezi miwili mnamo mwezi Novemba. 
Ramon Obey, mwandaaji mkuu wa kundi la kutetea haki za kiraia la People's Justice Project amesema, tukio hilo limeonyesha kuwa "mali ina thamani zaidi kuliko maisha ya mtu mweusi."
Katika miaka ya hivi karibuni, Marekani imeshuhudia maandamano makubwa ya kupinga ukatili mkubwa unaofanywa na polisi, ikiwa ni pamoja na mauaji ya 2020 ya George Floyd huko Minneapolis. Watetezi wa haki wameendelea kudai wahusika wa mauaji kuwajibishwa na kukomeshwa ubaguzi wa rangi dhidi ya Weusi.../
 
 
 

Tags