Maelfu ya wanawake waandamana dhidi ya Trump Marekani na Ulaya
Maelfu ya wanawake wameshiriki maandamano katika miji mikubwa ya Marekani na Ulaya kupinga sera za kibaguzi za Rais Donald Trump.
Nchini Marekani maandamano hayo makubwa yalishuhudiwa jana Jumamosi katika mji mkuu Washington na miji mikubwa ya nchi hiyo kama vile New York City, Boston, Houston, Los Angeles, San Francisco, Dallas, Philadelphia, Baltimore na Denver.
Aidha wanaharakati wanawake wamejitokeza kwa wingi katika maandamano hayo dhidi ya Trump katika miji mikubwa ya Ulaya, kama vile London, Geneva na Madrid.
Maandamano haya dhidi ya Trump hufanyika kila mwaka, ambapo washiriki huonesha kutoridhishwa kwao na sera za kibaguzi za Trump na hususan misimamo yake ya chuki na udhalilishaji dhidi ya wanawake, wahajiri na Wamarekani wenye asili ya Afrika.
Waandamanaji hao wanasema Trump ametumia mamlaka yake kuchochea hofu, ubaguzi wa kijinsia na chuki dhidi ya wageni na wahamiaji kwa ajili ya maslahi ya kisiasa.
Maandamano haya ya wanawake dhidi ya Trump yalifayika mara ya kwanza Januari 21 mwaka 2016, ikiwa ni siku moja tu baada ya kuanza kazi Trump katika Ikulu ya White House. Zaidi ya wanawake 66 elfu walishiriki maandamano hayo.