Aug 02, 2021 10:14 UTC
  • Mwanaharakati wa Ufaransa: Sheria ya karibuni dhidi ya Uislamu inahalalisha ubaguzi dhidi ya Waislamu

Mwanaharakati mmoja wa haki za binadamu wa nchini Ufaransa amesema kuwa sheria iliyopitishwa karibuni na bunge la nchi hiyo inahalalisha kisheria kufanyika ubaguzi dhidi ya Uislamu na Waislamu wa nchi hiyo.

Maria di Katrina, mwanaharakati wa haki za binadamu wa Ufaransa amesema katika mahojiano na shirika la habari la Anatoli kwamba lengo la serikali ya Paris katika kutekeleza sheria hiyo kwa kisingizio cha kulinda misingi ya usekulari, ni kuwalenga Waislamu wa nchi hiyo ya Ulaya na kuongeza kuwa sheria hiyo bila shaka itaongeza chuki na uadui dhidi ya Uislamu katika nchi hiyo ambayo ina idadi kubwa zaidi ya Waislamu barani Ulaya.

Katrina anasisitiza kuwa Ufaransa, kinyume na vinavyotangaza vyombo vya habari vya  nchi hiyo, ndiyo nchi iliyo na sheria mbaya na za chuki zaidi barani Ulaya dhidi ya Waislamu na wala wafuasi wa dini tofauti hawachukuliwi kuwa sawa mbele ya sheria na katiba ya nchi hiyo.

Rais Macron wa Ufaransa

Vipengee vya sheria hiyo vinawalenga Waislamu moja kwa moja na vinakusudia kufutilia mbali haki yao ya uhuru wa kuabudu.

Bunge la Ufaransa tarehe 23 Julai lilipitisha sheria tata na iliyo dhidi ya Uislamu ambayo iliwasilishwa bungeni na serikali ya Rais Emmanuel Macron kwa madai ya kulinda misingi ya usekulari nchini.

Wakosoaji wa sheria hiyo wanasema mbinu hiyo imetekelezwa na rais huyo mwenye chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu kwa ajili ya kumfanya ashinde katika uchaguzi wa rais uliopangwa kufanyika nchini humo baadaye mwaka huu.

Tags