Hizbullah: Magaidi wanaoungwa mkono na Saudia na US, hatari M/Kati
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i9895-hizbullah_magaidi_wanaoungwa_mkono_na_saudia_na_us_hatari_m_kati
Katibu Mkuu wa harakati ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon amesema makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono kwa hali na mali na Saudia na Marekani yanatishia usalama wa eneo hili la Mashariki ya Kati.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Jun 24, 2016 22:41 UTC
  • Hizbullah: Magaidi wanaoungwa mkono na Saudia na US, hatari M/Kati

Katibu Mkuu wa harakati ya Kiislamu ya Hizbullah ya Lebanon amesema makundi ya kigaidi yanayoungwa mkono kwa hali na mali na Saudia na Marekani yanatishia usalama wa eneo hili la Mashariki ya Kati.

Sayyid Hassan Nasrullah aliyasema hayo jana Ijumaa, katika maadhimisho ya Arubaini ya kamanda mwandamizi wa harakati hiyo ya muqawama, Shahidi Mustafa Badreddine aliyeuawa nchini Syria Mei 13 na kusisitiza kuwa, mwanamapambano huyo alikuwa mstari wa mbele katika mapambano dhidi ya utawala wa Kizayuni wa Israel na matakfiri wa Daesh. Amesema Saudia na Uturuki zimetuma maelfu ya wanachama wa Daesh nchini Syria kwa lengo la kuiangusha serikali halali ya Rais Bashar al-Assad lakini njama hizo zimeambulia patupu. Kadhalika Sayyid Hassan Nasrullah amekanusha madai ya kipropaganda yanayotolewa na vyombo vya habari vya Kiarabu kwamba Hizbullah inaelekea kusambaratishwa katika eneo la Aleppo nchini Syria na kuongeza kuwa, zaidi ya magaidi 600 wameuawa kaskazini magharibi mwa mji huo mwezi huu wa Juni pekee, katika operesheni ya pamoja ya harakati hiyo ya Muqawama na jeshi la Syria.

Itakumbukwa kuwa, Mustafa Badreddine, kamanda huyo wa Hizbullah aliyekuwa na umri wa miaka 55 aliongoza tawi la harakati hiyo ya Kiislamu lililokuwa linaisaidia serikali ya Syria katika vita dhidi ya magaidi. Aidha aliongoza oparesheni dhidi ya wanajeshi vamizi wa Israeli huko Lebanon na hivyo amekuwa akilengwa kuuawa kwa muda mrefu na Marekani, Israeli na waitifaki wao. Shahidi Badreddine alikuwa binamu yake Imad Mughniyeh ambaye naye aliuawa shahidi katika oparesheni iliyotekelezwa na utawala haramu wa Israel mjini Damascus, Syria mwaka 2008.